Tuesday, 4 February 2025

WANACHAMA WA CCM WILAYA YA SONGEA, VIJIJINI JIMBO LA MADABA WAMUNGAMO MKONO AZIMOAMKUTANO MKUU MAALUMU CCM TAIFA

 


Katika sherehe za miaka 48 ya kuzaliwa kwa Chama cha Mapinduzi (CCM), wanachama wa CCM kutoka Wilaya ya Songea Vijijini, Jimbo la Madaba, wakiongozwa na Mwenyekiti wao, Thomas Masolwa, wamepongeza na kuunga mkono Mkutano Mkuu Maalum wa CCM Taifa, uliopitisha azimio la kumteua Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kuwa mgombea wa urais kwa tiketi ya chama hicho katika Uchaguzi Mkuu wa 2025 kwa Tanzania Bara, huku Rais wa Zanzibar, Dkt. Hussein Ali Mwinyi, akiteuliwa kugombea urais kwa upande wa Zanzibar.



Akizungumza na wanachama wa CCM na wananchi wa Jimbo la Madaba waliojitokeza kusherehekea miaka 48 ya CCM katika kijiji cha Lutukila kilichopo kata ya Mkongotema, Masolwa alieleza furaha ya wanachama wa CCM Jimbo la Madaba kutokana na mafanikio makubwa yaliyofikiwa chini ya uongozi wa Rais Samia. Ametaja maendeleo katika sekta za afya, elimu, miundombinu, kilimo na huduma nyingine za kijamii ambazo zimeboresha maisha ya wananchi, hasa wa vijijini.

Aidha wanacha hao wamempongeza na kuunga mkono mwenyekiti wa chama hicho taifa kwa kumchagua Balozi Dkt. Emmanuel John Nchimbi, Katibu Mkuu wa CCM, kama mgombea mwenza katika uchaguzi ujao.

Masolwa amewataka Wananchi wa Jimbo la Madaba kuendelea kuiunga mkono CCM kwa kumchagua Rais Samia na viongozi ngazi ya ubunge na udiwani watakaoteuliwa na chama hicho kupeperusha bendera ya chama  katika uchaguzi ujao



Katibu wa CCM Wilaya ya Songea Vijijini, Juma Nambaila, amesema kuwa maadhimisho ya miaka 48 ya CCM yameambatana na shughuli mbalimbali za kijamii, zilizofanywa na jumuiya za chama ikiwemo upandaji miti, usafi wa mazingira, na uchangiaji damu,

Mbunge wa Jimbo la Madaba, Dkt. Joseph Mhagama, ameishukuru Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Samia kwa kutekeleza miradi ya maendeleo katika jimbo hilo. Amesema wananchi wa Madaba wanapata manufaa makubwa kutokana na serikali yao kupitia miradi mbalimbali ya maendeleo iliyotekelezwa na serikali ya chama cha mapinduzi ikiongozwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan

Sherehe hizi zimeonyesha mshikamano wa wanachama wa CCM, huku wakiahidi kuendelea kuiunga mkono CCM na Rais Samia katika kipindi cha uongozi wa Awamu ya Sita.

 


No comments:

Post a Comment